HOTUBA YA
MHESHIMIWA KASSIM M. MAJALIWA (MB), WAZIRI MKUU WA JAMHURI YA MUUNGANO WA
TANZANIA WAKATI WA KUHITIMISHA SHUGHULI ZA MKUTANO WA KUMI NA TISA WA BUNGE
1.
Mheshimiwa
Spika,
naomba nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujaalia
afya njema na kutuwezesha kufika siku hii ya leo ambayo naiita kuwa ni siku ya
kihistoria kwetu.
2.
Nasema kuwa ni ya kihistoria kwa sababu Bunge
lako Tukufu linahitimisha shughuli za Bunge la Kumi na Moja (11) la Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania pia tunahitimisha Mkutano wa Kumi na Tisa (19) wa Bunge
ulioanza mwezi wa Aprili mwaka huu wa 2020.
3.
Mheshimiwa
Spika,
katika Mkutano huu wa Bunge, licha ya uwepo wa ugonjwa wa homa ya mapafu
inayosababishwa na virusi vya Corona (COVID-19), tumeweza kukaa hapa Dodoma kwa
kipindi kisichopungua miezi miwili na nusu. Aidha, katika kipindi hicho
tumeweza kutekeleza majukumu yetu yote kama ilivyokuwa imepangwa.
4.
Ama kwa hakika hatuna budi kumshukuru Mwenyezi
Mungu kwani tunakamilisha maisha yetu ya Kibunge kwa kipindi cha miaka mitano
toka Novemba 2015. Tumeshirikiana katika maeneo mengi nje na ndani ya Bunge kwa
kila mmoja kutekeleza majukumu yake.
5.
Mheshimiwa
Spika,
siwezi kuanza kueleza yaliyojiri kwenye majukumu yetu bila kumshukuru Mwenyezi
Mungu aliyeniwezesha kuwa na afya njema na kunisimamia katika kila jambo na
hasa nilipokuwa natekeleza majukumu yangu binafsi na ya umma kwa kipindi chote
hadi sasa. InshaAllah, yeye ndiye msimamizi wa yote.
6.
Mheshimiwa
Spika,
kwa moyo mkunjufu kabisa naomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa
Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa
kitendo chake cha kuniamini na kuniteua kushika wadhifa wenye dhamana kubwa ya
kumsaidia kazi ya utendaji ndani ya Serikali kwa kipindi chote cha miaka mitano.
7.
Kwa niaba ya Familia yangu na Wana-Ruangwa
wote, namshukuru sana kwa ukarimu, imani na upendo aliouonesha kwetu, Mwenyezi
Mungu aendelee kumpa nguvu, ulinzi, kheri na kila lililo jema na aendelee
kuliongoza Taifa hili vyema na kwa mafanikio makubwa kama ambavyo Watanzania
tumeendelea kushuhudia mafanikio makubwa katika kipindi hiki cha Uongozi wake wa
Awamu ya Tano.
8.
Mheshimiwa
Spika,
Rais wetu ametenda mema kwa Watanzania na watamlipa mema. Ninamwombea kheri pia
kwa Uchaguzi Mkuu ujao ashinde kwa ushindi wa kishindo. Amina.
9.
Mheshimiwa
Spika,
ninamshukuru sana pia Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano wake mkubwa wakati wote
nikitekeleza majukumu ya Waziri Mkuu. Vilevile, ninashukuru sana kwa
ushirikiano mkubwa nilioupata kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein,
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Mheshimiwa Balozi Seif
Ali Iddi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar pamoja na viongozi, watendaji na
wananchi wote wa Zanzibar.
10.
Mheshimiwa
Spika,
nitumie nafasi hii pia kukushukuru sana wewe binafsi kwa upendo uliouonesha
kwangu kipindi chote cha uhai wa Bunge la Kumi na Moja (11). Kwa uzoefu ulionao
katika kuendesha Bunge, umekuwa msaada sana kwangu kwa kunipa ushauri na
ushirikiano wa dhati ulionifanya nijenge imani kubwa kwenye majukumu yangu
ndani ya Bunge.
11.
Mheshimiwa
Spika,
nami niungane na wenzangu kukutakia kheri nyingi kwenye Uchaguzi ujao, naamini
Wana-Kongwa watasikiliza na kutekeleza dua zetu za kuwa upite bila kupingwa, na
ukirudi hapa chukua fomu ya Uspika ili upate kura zote za ndiyo uendelee kuwa
Spika wa Bunge la Kumi na Mbili (12).
12.
Mheshimiwa
Spika,
sitasahau tukio la tarehe 19 Novemba, 2015 siku ambayo Mheshimiwa Dkt. John
Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipowasilisha jina
langu katika Bunge lako Tukufu na kupendekeza niwe Waziri Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania.
13.
Mheshimiwa
Spika,
nakushukuru tena wewe na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa imani mlioionesha kwa
kuridhia mapendekezo ya Mheshimiwa Rais na kunipigia kura nyingi za ndiyo na
mkaridhia tufanye kazi kwa pamoja katika kuwatumikia Watanzania.
14.
Waheshimiwa
Wabunge wenzangu, natambua, naheshimu na nathamini ushirikiano
wa dhati mlionipa katika kipindi chote cha Bunge. Nami nawaombea na nawatakia
ushindi wa kishindo kwenye Majimbo yenu ili mrudi tena hapa mwezi Novemba,
2020.
15.
Mheshimiwa
Spika,
pia, nawashukuru sana Mheshimiwa Dkt. Tulia Akson, Naibu Spika, Wenyeviti wa
Bunge Mheshimiwa Mtemi Andrew Chenge, Mheshimiwa Najma Murtaza Giga na
Mheshimiwa Mussa Zungu Azzan ambaye mwishoni alipata uteuzi wa Mheshimiwa Rais
kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira kwa kuliongoza Bunge hili
kwa busara na umahiri mkubwa.
16.
Mheshimiwa
Spika,
vilevile, namshukuru Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki, Mbunge wa Maswa
Magharibi na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti pamoja na
Wajumbe wote wa Kamati hiyo kwa mchango wao mkubwa katika kufanikisha Bajeti ya
Serikali. Pia, nawashukuru Katibu wa Bunge Ndugu Stephen Kagaigai na Watumishi
wote wa Bunge kwa ushirikiano mkubwa waliotupatia katika Mkutano huu na Mikutano
iliyoendeshwa kipindi chote cha miaka mitano.
17.
Mheshimiwa
Spika,
katika kutekeleza majukumu ya Ofisi ya Waziri Mkuu hapa Bungeni, napenda kutambua
mchango wa Mheshimiwa Jenista Joakim Mhagama (Mb), Waziri wa Nchi, Ofisi ya
Waziri Mkuu anayesimamia Sera, Uratibu, Bunge, Ajira, Kazi, Vijana na Watu
wenye ulemavu. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mhagama kwa kunisaidia
ipasavyo katika kutekeleza majukumu yangu sambamba na majukumu yake ya unadhimu
na uratibu wa shughuli za Serikali Bungeni. Nakuombea sana kwa wananchi wa
Peramiho, Maposeni, Mgazini, Mdunduwalo, wakupitishe upite bila kupingwa.
18.
Mheshimiwa
Spika, vilevile, namshukuru Mheshimiwa Angela Kairuki
(Mb), Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Uwekezaji kwa
kufuatilia na kusimamia hatua mbalimbali za kuimarisha na kuboresha mazingira
ya uwekezaji nchini. Mheshimiwa Waziri Kairuki amekuwa akitembelea maeneo
mbalimbali na kukutana na Wawekezaji wadau wa sekta binafsi ili kusikiliza
changamoto zao na kuzitafutia ufumbuzi. Juhudi zake hizo, zimekuwa na mchango
mkubwa katika kuboresha mazingira ya biashara na kuimarisha mahusiano ya sekta
binafsi na Serikali nchini. Nawe nakutakia kila la kheri huko uendako ili upate
kura za kutosha.
19.
Mheshimiwa
Spika, kwa
upande wa masuala ya maendeleo na uwezeshaji wa vijana napenda kumshukuru
Mheshimiwa Anthony Peter Mavunde, Mbunge wa Dodoma Mjini, Naibu Waziri wa Nchi
Ofisi ya Waziri Mkuu kwa msaada mkubwa katika kusimamia vizuri masuala ya
vijana na ajira. Kadhalika, namshukuru Dada yangu Mheshimiwa Stella Ikupa Alex
(Mb), Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kusimamia vema masuala na maslahi
ya Watu Wenye Ulemavu.
20.
Nawashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri wenzangu
na Naibu Mawaziri; Professor Adelardus Kilangi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali; Balozi
Mhandisi John William Kijazi, Katibu Mkuu Kiongozi; Makatibu Wakuu na Naibu
Makatibu Wakuu wakiongozwa na Bw. Tixon Tuyangine Nzunda, Andrew Wilson Massawe,
na Bibi Dorothy Aidan Mwaluko kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu. Nawashukuru kwa
ushirikiano wa dhati mlionipa katika kuratibu na kusimamia shughuli za Ofisi ya
Waziri Mkuu. Bila kuwasahau Watendaji wote wa Ofisi ya Waziri Mkuu.
21.
Mheshimiwa
Spika,
nitumie fursa hii pia kuwashukuru Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama akiwemo
Jenerali Venance Mabeyo - Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama; Inspekta
Jenerali wa Polisi - Simon Nyakoro Sirro; Brigedia Jenerali Suleiman Mzee
-Kamishna Jenerali wa Magereza; Dkt. Anna Makakala - Kamishna Jenerali wa
Uhamiaji; John William Hasunga - Kamishna Jenerali wa Zimamoto na Uokoaji; Kamishna
Diwani Athumani - Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa; Brigedia Jenerali John
Mbung’o - Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa; James Kaji - Kamishna
Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Madawa ya Kulevya.
Wakuu hao wa Vyombo vya Ulinzi na
Usalama wameonesha nidhamu na uzalendo mkubwa katika kuhakikisha Nchi yetu,
raia wake na mali zao wanakuwa salama.
22.
Mheshimiwa
Spika,
nawashukuru pia Wakuu wa Taasisi, Wakurugenzi na Watendaji wote Serikalini kwa
ushirikiano mzuri walioutoa na utendaji wa pamoja wenye mafanikio makubwa.
Aidha, tuendelee kutakiana mema na tuchape kazi hadi hapo utumishi wetu
utakapokoma.
23.
Mheshimiwa
Spika,
nimalizie salamu zangu za shukrani kwa Familia yangu ambayo inaniunga mkono,
kunivumilia pale ambapo nawatumikia Watanzania na kunitia moyo siku hadi siku
kwenye majukumu yangu. Bila kuwasahau Wana-Ruangwa ambao walinipigia kura bila
kujali Vyama vyao na kuniwezesha kuingia Bungeni na hatimaye nikapata uteuzi wa
Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa ajili ya kuwatumikia
Watanzania. Nataka niwahakikishie Wana-Ruangwa kuwa bado tuko pamoja katika
harakati za kuleta maendeleo. Nawashukuru sana.
24.
Mheshimiwa
Spika,
nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitawashukuru wananchi na Watanzania wote kwa
kuiunga mkono Serikali ya Awamu ya Tano na ushirikiano walioutoa kwa Serikali
wakati wa utekelezaji wa shughuli mbalimbali za maendeleo ya Taifa kwa ujumla
bila kujali tofauti zao za kiitikadi au dini. Sambamba na kuonesha uzalendo,
mshikamano na kudumisha amani na utulivu uliowezesha Serikali kutekeleza
majukumu yake kwa ufanisi na weledi, kwa mujibu wa taarifa zinazotolewa na
taasisi ya GLOBAL PEACE INDEX 2020 inayofuatilia masuala ya amani duniani.
Tanzania ni nchi ya saba kwa amani na utulivu Afrika na ni nchi ya kwanza kwa amani Afrika Mashariki.
Naamini wananchi wataendelea kuiunga mkono Serikali yetu ili ifanye mambo
makubwa zaidi katika kipindi cha pili cha Awamu ya Tano kwa amani na maendeleo
yake.
25.
Mheshimiwa
Spika,
baada ya salamu za shukurani nami naungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu
walionitangulia kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Mbunge wa
Iramba Magharibi kwa kuteuliwa kuwa Waziri wa Katiba na Sheria na Mheshimiwa
Dkt. Godwin Aloyce Mollel, Mbunge wa Siha kwa kuteuliwa kuwa Naibu Waziri wa
Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.
Aidha, mkiwa viongozi
mlioteuliwa, tambueni kuwa mnalo jukumu kubwa la kuwahudumia Watanzania,
hususan katika kipindi hiki ambacho Nchi yetu imekumbwa na changamoto
mbalimbali likiwemo janga la Corona.
SALAMU ZA POLE
26.
Mheshimiwa Spika, wakati tukiendelea na Mkutano huu wa 19, Bunge lako Tukufu lilipata pigo
kwa kuondokewa na Wabunge wenzetu akiwemo Mheshimiwa Mchungaji Dkt. Getrude
Pangalile Rwakatare, aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum; Mheshimiwa Richard Mganga
Ndassa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Sumve na Mheshimiwa Balozi Dkt. Augustine
Philip Mahiga, aliyekuwa Mbunge na Waziri wa Katiba na Sheria.
27.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi hicho pia, tuliondokewa na aliyekuwa Jaji Mkuu Mstaafu,
Mheshimiwa Jaji Augustino Ramadhan. Aidha, niungane na Mheshimiwa Dkt. John
Pombe Magufuli kuwapa pole majirani zetu, wananchi wa Burundi kwa kifo cha
aliyekuwa Rais wa Nchi hiyo, Mheshimiwa Pierre Nkurunzinza. Tuendelee kumuomba
Mwenyezi Mungu azipumzishe Roho za wapendwa wetu wote mahali pema. Amina.
28.
Mheshimiwa Spika, vilevile, Taifa letu lilikumbwa na majanga mbalimbali ikiwa ni pamoja na
mafuriko, COVID-19 na ajali za barabarani ambazo zilisababisha vifo, majeruhi
na uharibifu wa mali. Napenda kutoa salamu za pole kwa ndugu, jamaa na marafiki
waliopoteza wapendwa wao na wengine kupata majeraha kutokana na matukio hayo. Tumuombe
Mwenyezi Mungu aziweke Roho za marehemu mahali pema na waliopata majeraha
awajalie nafuu na kupona mapema. Amina.
MAFANIKIO
YA SERIKALI YA AWAMU YA TANO
29.
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee kabisa nitumie
fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania kutokana na fikra na uongozi makini katika ujenzi wa
Taifa letu. Ni dhahiri kuwa maono yake katika kuongoza na kusimamia utekelezaji
wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015 - 2020 na mipango ya Serikali, zimeleta mafanikio
makubwa ambayo hivi sasa wote tunayaona.
30.
Mheshimiwa Spika, nyote mtakubaliana nami kwamba Mheshimiwa Rais na Makamu wake Mheshimiwa
Samia Suluhu Hassan, wamekuwa mstari wa mbele kuhakikisha wanawafikia
Watanzania, wanawasikiliza na kutatua kero zao. Lengo la ziara hizo, pamoja na
mambo mengine lilikuwa ni kusimamia utekelezaji wa maelekezo ya Ilani ya Chama
cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2015 ikiwemo kukagua miradi ya maendeleo;
kuzungumza na watumishi na kuwafahamisha kuhusu falsafa ya Serikali ya awamu ya
tano ya Hapa Kazi Tu.
31.
Mheshimiwa Spika, ziara hizo zimesaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha utendaji wa watumishi
wa umma. Hivi sasa, wananchi wanapokwenda katika ofisi za umma wanapokewa,
wanasikilizwa na kuhudumiwa vizuri. Aidha, usimamizi wa miradi ya maendeleo umeimarika
sambamba na kuakisi thamani halisi ya fedha katika utekelezaji wa miradi hiyo.
Hapa Bungeni ninawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa maoni, ushauri na
ushirikiano ambao mmekuwa mkiutoa wakati wa ufuatiliaji wa shughuli za
maendeleo sambamba na kuisimamia Serikali yetu.
Mambo mengi ya kujivunia yamefanywa na tumekuwa tukiyaeleza katika maeneo
mengi kupitia mikutano ya hadhara, vyombo vya habari, nyaraka mbalimbali, uwepo
wa miradi mingi ya kimkakati hadi kwa wananchi wa kawaida.
32.
Nitaeleza majukumu
na miradi michache tena kwa kifupi ili kuwakumbusha nini Serikali imefanya
katika kipindi hiki cha miaka mitano.
·
Marekebisho ya
nidhamu kwa utumishi wa umma na uwajibikaji Serikalini ili kuwezesha Watumishi
kutambua majukumu yao na kuwatumikia Watanzania.
·
Mapambano dhidi ya rushwa
ndani ya Serikali na nje ya Serikali ili kulinda mali na fedha za umma. Hatua
hii ni endelevu, lengo ni kung’oa mizizi ya rushwa nchini.
·
Kuimarisha vyombo
vya ulinzi na usalama, mhimili wa Bunge na Mahakama. Matakwa yetu ni kuhakikisha
kuwa nchi inabaki salama na mihimili ifanye kazi yake.
·
Mapambano dhidi ya
matumizi ya dawa za kulevya ili kujihakikishia kuwa tunakuwa na Taifa lenye
nguvukazi inayofanya kazi. Mapambano bado yanaendelea. Tutapambana na
wazalishaji, wasambazaji, wauzaji na watumiaji wa dawa za kulevya.
·
Utambuzi wa
watumishi hewa waliokuwa wanalipwa fedha wakiwa hawapo. Katika zoezi hili tumepata mafanikio makubwa na
kuokoa shilingi Bilioni 19.83 kwa kuwaondoa kwenye mfumo wa malipo
watumishi hewa 19,708 na wenye vyeti vya kugushi 15,411.
·
Ukusanyaji wa mapato
ili kuwezesha Serikali kujenga miradi na kutoa huduma muhimu. Ukusanyaji
wa mapato umeongezeka kutoka wastani wa shilingi Bilioni 800 kwa mwezi mwaka
2015 hadi wastani wa shilingi trilioni 1.5 kwa mwezi katika kipindi
cha Julai 2019 hadi Aprili 2020.
·
Kuimarisha uwekezaji
kwa kujenga viwanda. Hadi Aprili 2020 jumla ya viwanda vipya 8,477
vikiwemo vidogo, vya kati na vikubwa vimeanzishwa katika maeneo mbalimbali
nchini na hivyo kuwezesha ongezeko la ajira viwandani za viwandani zipatazo
482,601.
·
Kuimarisha kilimo na
masoko. Tumeimarisha kilimo cha mazao makuu, kama vile, Korosho, Pamba, Chai, Tumbaku,
Kahawa, Michikichi na Mkonge pamoja na mazao ya chakula ili kuwa na uhakika wa
usalama wa chakula.
·
Kuimarisha ushirika wa
kilimo na upatikanaji wa pembejeo pamoja na huduma za ugani ili kuwafanya
wakulima kuzalisha kwa tija.
·
Marekebisho ya Sheria ya madini yamefanyika
sambamba na kuanzisha masoko ya madini 28 na vituo 12 vya ununuzi wa madini
katika maeneo ya uchimbaji na hivyo kuongeza makusanyo ya Serikali, kupungua
biashara haramu na utoroshaji madini kwenda nje. Mwezi Machi hadi Septemba,
2019 jumla ya kilo za dhahabu 4,680.28 zenye thamani ya shilingi bilioni 432.49
zimezalishwa na Serikali kukusanya shilingi bilioni 30.27.
·
Kuhamishia Makao
Makuu Dodoma ambapo tayari Watumishi wapatao 15,361 wamehamia Dodoma na
sasa fursa za uwekezaji zimeongezeka katika Jiji la Dodoma.
·
Kuboresha miundombinu
na taaluma Sekta ya Elimu kwa ngazi zote kuanzia awali hadi Elimu ya Juu
ikiwemo ujenzi na ukarabati wa madarasa, maktaba, maabara, nyumba za walimu,
mabweni na ukarabati wa shule kongwe ili kuziongezea uwezo wa kupokea wanafunzi
wengi zaidi.
·
Sera ya Elimu bila Ada
ambayo inatumia zaidi ya Shilingi Bilioni 20.8 kila mwezi kwa ajili ya fidia ya
ada, posho ya madaraka kwa walimu wakuu, wakuu wa shule na waratibu kata kila
mwezi toka 2016 na tutaendelea. Hii imesaidia kuongeza uandikishaji na
mahudhurio shuleni.
· Kuimarisha huduma za afya kwa kujenga Zahanati, Vituo vya Afya, kujenga
Hospitali za Wilaya, Mikoa, Kanda na za Kitaifa, huduma za Madawa na Vifaa Tiba.
Tumejenga Zahanati 1,198 Vituo vya Afya 487, Hospitali za Wilaya 71,
Hospitali za Rufaa za Mikoa 10, na Hospitali za Kanda 03 za
Kusini – Mtwara, Magharibi – Tabora na Kanda ya Ziwa - Burigi.
· Ujenzi wa miradi ya maji Vijijini na Mijini tumefikia asilimia 84
Mijini na asilimia 70.1 Vijijini.
· Ufufuaji wa Shirika la Ndege kwa kununua ndege kumi na moja (11) ambazo
zinatoa huduma mikoa yote yenye Viwanja vya Ndege na nje ya nchi.
· Ujenzi na ukarabati wa Viwanja vya Ndege kwenye mikoa isiyo na Viwanja
vya Ndege unaendelea.
· Ununuzi wa Rada nne mpya za kuongoza Ndege za kiraia zilizo Mwanza,
Mbeya, Dar-es-Salaam na Kilimanjaro.
· Ujenzi wa mradi mkubwa wa kufua umeme (Mwalimu Nyerere Dam) utakaozalisha
Mg 2115 kwa sasa umefikia asilimia 40. Ujenzi una gharama ya Shilingi Trilioni
6.5
· Usambazaji wa umeme Vijijini kupitia Wakala wa Nishati
Vijijini (REA) tumefikia Vijiji kwa asilimia
80% ambapo hadi Aprili 2020 shilingi trilioni 2.27 zimetumika na kufanikisha
jumla ya vijiji 9,112 kati ya 12,268 vya Tanzania Bara kuunganishwa na umeme
kutoka vijiji 2,118 mwaka 2015.
· Ujenzi wa Mradi
wa Reli ya Kimataifa (SGR) wa Kilomita 300
Dar-es-Salaam–Morogoro. Mradi umefikia asilimia 78. Kipande cha Morogoro hadi
Makutupora Kilomita 422 mradi umefikia asilimia 30 ya kazi. Lengo ni
kukamilisha mradi huu ifikapo Juni 2021 kwa gharama ya Shilingi Trilioni 7.5.
·
Ujenzi wa Barabara kwa kiwango cha lami zikiwemo barabara kuu, barabara za mikoa na za
wilaya zenye thamani ya
zaidi ya Shilingi Trilioni 7.6. Pia serikali inaendelea kujenga barabara ya
njia nne kutoka kutoka Kimara hadi Kibaha (km 19.2)
· Ujenzi wa madaraja: ujenzi wa
daraja la juu la Mfugale (Dar-es- Salaam), daraja la Furahisha (Mwanza) na
daraja la Magufuli (mto Kilombero) umekamilika; ujenzi wa barabara ya pete (Ubungo
interchange) umefikia asilimia 77 kwa shilingi bilioni 247; Aidha, ujenzi unaendelea kwa daraja la New Selander
(Dar- es-Salaam) kwa shilingi Bilioni 270. Daraja la Kigongo- Busisi shilingi
Bilioni 699.2
· Ujenzi wa
Bandari, uboreshaji na upanuzi wa Bandari za Tanga,
Dar-es-Salaam na Mtwara kwa Shilingi zaidi ya Trilioni 1.2. Pia, ujenzi wa
Bandari ya Kigoma na Kalema umeshatengewa fedha.
· Ujenzi wa Meli mpya yenye uwezo
wa kubeba abiria 1,200 na tani 400 za mizigo katika Ziwa Victoria na ujenzi wa
chelezo; ukarabati wa meli ya MV Victoria na MV Butiama ambapo katika kipindi
cha mwaka 2015/16 hadi Aprili, 2020 jumla ya shilingi bilioni 111.7 zimetumika.
Vile vile, Serikali
imekamilisha ujenzi wa meli moja mpya yenye uwezo wa kubeba abiria 200 na tani
200 za mizigo katika Ziwa Nyasa; na ukarabati wa meli ya mafuta ya MT Sangara
katika Ziwa Tanganyika.
· Ujenzi wa
Vivuko vya MV Kigamboni, MV Pangani, Kigongo -Busisi, MV Sengerema na
Nyamisati.
· Urejeshaji na usimamizi wa mali za Ushirika zilizokuwa zimechukuliwa
kinyume na utaratibu, kama vile, NYANZA, SHIRECU, KNCU, Mamlaka ya Mkonge
Tanzania, n.k.
· Kusimamia maboresho kwenye Sekta ya Uvuvi na Mifugo kwa kuvua na kufuga kisasa,
kujenga viwanda na masoko yake.
33.
Mheshimiwa
Spika, Serikali ya Chama cha Mapinduzi kupitia Bunge lako
Tukufu katika kipindi cha miaka minne imeidhinisha jumla ya shilingi
trilioni 33.1 kwa ajili ya utekelezaji wa
miradi ya maendeleo kote nchini ikiwemo miradi ya kimkakati niliyoitaja hivi
punde
MVUA KUBWA
ZILIZONYESHA NCHINI
34.
Mheshimiwa
Spika,
baadhi ya maeneo ya Nchi yetu yalikumbwa na mafuriko kufuatia mvua nyingi
zilizonyesha nchini. Mafuriko hayo yalisababisha madhara mbalimbali ikiwemo
uharibifu wa miundombinu, mali na vifo. Serikali imeendelea kuchukua hatua za
kurejesha hali ya miundombinu iliyoharibika na zoezi hilo ni endelevu.
35.
Mheshimiwa
Spika,
mvua nyingi tulizopata msimu huu zimeleta neema ya mavuno lakini pia katika
baadhi ya maeneo mazao yameharibika. Hivyo, niendelee kusisitiza kauli ya
Waziri wa Kilimo wakati akiwasilisha Hoja ya Wizara yake kuwa hali ya chakula
nchini imeendelea kuimarika. Kwa msingi huo, hatutarajii kuwa na upungufu
wowote wa chakula kwa msimu ujao. Muhimu kwetu ni kuongeza umakini wa matumizi
kwa kuweka akiba ya chakula ili kitosheleze mahitaji ya familia hadi msimu
ujao.
MAPAMBANO DHIDI YA
HOMA KALI YA MAPAFU COVID 19
36.
Mheshimiwa Spika, mwezi Machi, 2020, baada ya Shirika la Afya Duniani (WHO)
kutangaza kuwa COVID 19 ni janga la dunia, ambako nchi nyingi duniani zilipata
maambukizi makubwa, Tanzania tulitangaza kisa cha kwanza tarehe 15 Machi, 2020.
37.
Nchi nyingi duniani zikiwemo nchi za Bara la
Afrika ugonjwa huu ulianza kuingia. Kila nchi ilichukua hatua kadhaa za
kudhibiti maambukizi zikiwemo watu kutotoka ndani ya nyumba zao “Lockdown”, kuzuia mikusanyiko kwa
kufunga mashule, vyuo, michezo, aina zote za usafiri wa ndani na nje, maeneo ya
Ibada na shughuli za uzalishaji maeneo ya kazi, viwanda, n.k. vilifungwa.
38.
Tanzania nasi tulianza kuchukua hatua kadhaa
ili kukabiliana na maambukizi kwa kuunda Kamati 3 za ngazi ya Mawaziri,
Watendaji na Wataalam wa Afya kwa lengo la kufanya tathmini ya hatua za
kuchukua ili kupunguza maambukizi na kulinda anguko la kiuchumi.
39.
Hatua zilizochukuliwa ni kupunguza misongamano
kwa kufunga shule, vyuo, mikutano, kunawa maji, matumizi ya vitakasa mikono na
kuvaa barakoa.
40.
Mheshimiwa
Spika,
siku ya tarehe 22 Machi, 2020 Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa Jijini Dodoma na tarehe 03 Mei, 2020
akiwa Chato aliwataka Watanzania kuwa watulivu waondoe hofu ya ugonjwa huu na
ni ugonjwa kama magonjwa mengine, kama vile Malaria, UKIMWI, Kifua Kikuu, n.k.
na kuwataka Watanzania kuchukua tahadhari na kuendelea na shughuli za
uzalishaji mali, kufanya kazi ofisini, viwandani, mashambani na kutofunga
nyumba za Ibada.
41.
Mheshimiwa
Spika,
Mheshimiwa Rais alihutubia tena Taifa tarehe 16 Aprili, 2020 kwa kutoa maelekezo
na kusisitiza yafuatayo:
Mosi: Aliwasihi Watanzania kuondoa hofu kwa
kuwa Mungu yupo nasi na hivyo, waendelee kuchapa kazi ili kunusuru uchumi wa
mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla na kuzingatia kanuni za afya.
Pili: Watanzania watumie
siku tatu kumuomba na kumlilia Mwenyezi Mungu kwani Mungu yu pamoja nasi na
atatusikia huku akiendelea kusimamia kauli yake ya kuwataka Watanzania wafanye
kazi kwa bidii na kumtegemea Mungu bila kujali kauli za kebehi na ukosoaji
kutoka pande mbalimbali za dunia;
Tatu: Alihimiza Watanzania kumtegemea
Mwenyezi Mungu na kwamba Mwenyezi Mungu pekee ndiye atakayetuvusha na
kutuepusha na janga hili;
Nne: Aliwahimiza Watanzania kutopuuza
umuhimu wa tiba mbadala katika mapambano dhidi ya COVID-19. Kauli hii, imekuwa
chachu katika kuimarisha tafiti za dawa za asili ambazo zimekuwa na mchango
mkubwa katika kupambana na maradhi mbalimbali ikiwemo COVID-19; na
Tano: Tarehe 20 Mei, 2020 akiwa Singida,
aliwaomba Watanzania watumie siku tatu kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa maajabu
aliyoyafanya kwa Taifa letu kwa kutuepusha kusambaa kwa virusi vya COVID-19.
42.
Mheshimiwa
Spika,
hali iliyoko sasa, ni kuwa maambukizi yamepungua na wagonjwa wamepungua
hospitalini. Kama kuna anayestahili sifa ni Mheshimiwa Dkt. John Pombe
Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa msimamo wake usiotetereka
na maono ya mbali aliyokuwa nayo yamekuwa chachu katika kupunguza maambukizi ya
COVID-19 na kulinda uchumi wa Nchi. Mheshimiwa Rais ameifanya Tanzania kuwa ya
kupigiwa mfano duniani kwa namna alivyoshughulikia ugonjwa huu.
43.
Mheshimiwa
Spika,
pongezi maalum kwa Viongozi wa dini kwa namna walivyoshirikiana na waumini
katika mapambano ya ugonjwa wa COVID-19. Wakati wote Viongozi hao wamekuwa
wakiwapatia waumini (Watanzania) faraja pia na wagonjwa kwamba Mwenyezi Mungu
atawaponya. Hatua hizo zimekuwa mhimili mkubwa wa upendo, umoja, mshikamano na
ujasiri miongoni mwa Watanzania. Tunawashukuru sana.
44.
Mheshimiwa
Spika,
taarifa iliyotolewa na Taasisi ya Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo (Organisation
for Economic Cooperation and Development - OECD) inabashiri kuwa kitendo cha
kuwafungia watu ndani yaani “Lockdown” kumesababisha vifo kwa njaa na kusinyaa kwa uchumi wa nchi
zilizoendelea kwa asilimia 2 kila mwezi.
45.
Mheshimiwa
Spika,
hivi sasa, nchi nyingi zinakubaliana kuwa “Lockdown”
si hatua sahihi ya kukabiliana na COVID-19. Vilevile, kisayansi inakadiriwa
kuwa nchi ambazo ziliwafungia watu wake na mipaka yake zipo katika hatari ya
kukumbwa na madhara makubwa ya ugonjwa huo pindi utakapotokea mlipuko wa pili
na hata wa tatu.
46.
Mheshimiwa
Spika,
kwa mantiki hiyo, mtizamo na hatua zilizochukuliwa na Tanzania katika kupambana
na COVID-19 zinaonesha upekee tulionao kama nchi. Serikali, inayo kila sababu ya kuwapongeza Watanzania ambao si tu
walipokea maelekezo ya Serikali lakini pia walifanya hivyo kwa uaminifu mkubwa
na kwa hiari yao wenyewe bila kushurutishwa na mamlaka yoyote ya nchi.
47.
Mheshimiwa
Spika,
nitumie fursa hii kuwashukuru wataalamu wetu wa afya kwa kuwahudumia wagonjwa
wa COVID19. Wataalamu wetu hao, walitekeleza majukumu yao bila kujali hatari ya
virusi hivyo kwa maisha yao na wapendwa wao. Vievile, naishukuru sekta binafsi,
mtu mmoja mmoja na wadau wote ambao waliitikia wito wa Serikali kwa kutoa
michango ya hali na mali katika kufanikisha vita dhidi ya COVID19 nchini.
Kipekee, niwashukuru wamiliki wa viwanda ambao waliitikia wito wa Mheshimiwa
Rais na kuanza kuzalisha vifaa kinga hapa nchini badala ya kuagiza nje waende
kufanya hivyo.
48.
Mheshimiwa
Spika,
ni matumaini yetu kwamba zile nchi zilizoondoa vizuizi sasa zinalo somo la
kujifunza kutoka Tanzania. Aidha, suala la kudhibiti maambukizi ya COVID 19
litaendelea kuwa kipaumbele cha Serikali kwa sasa sambamba na malengo ya muda
mrefu ya kumaliza ugonjwa huo hususan katika kipindi hiki ambacho Shirika la
Afya Duniani (WHO) nalo limebainisha kwamba COVID 19 si gonjwa la kuondoka mara
moja. Hivyo, watu na dunia kwa ujumla hatuna budi kujifunza namna ya kuishi na
virusi hivyo kama ilivyo kwa UKIMWI na virusi vingine, huku tukifanya kazi ili
kujiletea maendeleo.
49.
Mheshimiwa Spika, tarehe 9 Juni Bunge
lako Tukufu lilipitisha Azimio la kumpongeza na kumuunga mkono Mheshimiwa Dkt.
John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna
alivyomudu kuivusha nchi katika janga la COVID-19. Waswahili husema mnyonge
mnyongeni, haki yake mpeni. Katika hili, nami naomba niseme kidogo kwa kumpongeza
Mheshimiwa Rais kwa hotuba zake zote zilizohusu ugonjwa huu ambapo alihimiza
masuala muhimu kwa Watanzania katika kukabiliana na janga hili na zilitibu hofu
kubwa iliyokuwa imetanda kwa Watanzania.
50.
Mheshimiwa
Spika,
leo tunaona idadi ya wagonjwa wanaougua inapungua sana. Kwa mfano, taarifa ya
leo, Jumatatu tarehe 15 Juni, 2020 kutoka katika Vituo vya kutolea huduma na Hospitali
za Serikali na Binafsi nchini, inaonesha kuwa tuna wagonjwa 75 katika Mikoa 12
na Mikoa 14 haina wagonjwa ikiwemo Mkoa wa Dodoma, Geita, Kagera, Katavi,
Kigoma, Lindi, Mara, Manyara, Pwani, Rukwa, Ruvuma, Simiyu, Songwe na Tabora.
Pamoja na mwenendo huu, ninawaomba wananchi wote kuendelea kuchukua tahadhari
zote za kiafya na miongozo inayotolewa na Serikali.
51.
Nampongeza sana Mheshimiwa Ummy Mwalimu (Mb), kwa
kazi kubwa aliyoifanya usiku na mchana kuhakikisha kuwa maambukizi yanapungua
kwa kasi. Tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa hatua tuliyofikia. Pia, nawashukuru Katibu
Mkuu, Mganga Mkuu wa Serikali na Watendaji wote wa Wizara ya Afya kwa usimamizi
wa tatizo hili na naamini mnaendelea vema. Hongereni sana.
SHUGHULI ZILIZOTEKELEZWA
KATIKA BUNGE LA 11 (2015–2020)
52.
Mheshimiwa Spika, wakati Bunge la 11 likielekea kuhitimisha shughuli zake, limefanikiwa
kutekeleza masuala mbalimbali ikiwemo kujibu maswali na hoja zilizowasilishwa
na Waheshimiwa Wabunge; kujadili na kupitisha Miswada ya Serikali; Maazimio
mbalimbali yenye kuhusisha Mikataba na Itifaki za Kikanda na Kimataifa; kupokea
kauli za Serikali kuhusu ufafanuzi wa mambo mbalimbali pamoja na kuunda Tume
kwa ajili ya kufuatilia masuala muhimu yenye maslahi mapana kwa Taifa letu.
Maswali na
Majibu
53.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi chote
cha Bunge la 11 linaloelekea
kuhitimisha uhai wake tarehe 16 Juni, 2020 jumla ya maswali ya msingi 3,962 yameulizwa na Waheshimiwa Wabunge
na kujibiwa na Serikali. Aidha, maswali ya nyongeza 9,563 yameulizwa kutokana na maswali ya msingi na kujibiwa na
Serikali. Vilevile, jumla ya maswali 178
ya kawaida na ya nyongeza 162 yameulizwa
na Wabunge na kujibiwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu kupitia utaratibu wa maswali
ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu.
54.
Mheshimiwa
Spika,
kupitia Mkutano huu wa Kumi na Tisa, jumla ya maswali 471 ya msingi na mengine 69 ya
nyongeza yaliulizwa na Waheshimiwa Wabunge na kupatiwa majibu na Serikali.
Miswada,
Maazimio ya Bunge na Kauli za Serikali
Loading...
Usipitwe na Habari Yoyote. Install Mpekuzi App kwenye Simu Yako Upate Habari Zetu kwa Wepesi Zaidi
==>>... << BOFYA HAPA Kui Install>>
Mgid
hapa
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )